Alhamisi, 13 Aprili 2017

ATHARI ZA MATUMIZI YA DAWA ZA KULEVYA


MADHARA YA DAWA ZA KULEVYA:
Matumizi na biashara ya dawa za kulevya yameendelea kusababisha madhara makubwa mbalimbali nchini yakiwemo ya kiafya, kijamii, kiuchumi, kimazingira, kisiasa na kiusalama.

KIAFYA:
Dawa za kulevya zimeendelea kuleta madhara makubwa kiafya yakiwemo magonjwa ya akili, utegemezi wa dawa za kulevya, magonjwa ya mapafu, moyo, ini na figo. Aidha, matumizi ya dawa za kulevya yaliendelea kusababisha vifo vya ghafl a hasa miongoni mwa wajidunga kutokana kuzidisha dozi. Pia, matumizi ya dawa hizo yameendelea kuchangia kuenea kwa maambukizi ya VVU, kifua kikuu na virusi vya homa ya ini aina ya B na C. Watumiaji wengi wameendelea kukabiliwa na magonjwa ya meno na ngozi yakiwemo majipu, vidonda na ukurutu. Dawa za kulevya zimeendelea kusababisha kupungua kwa nguvu za kiume, ugumba, utasa na kuzaliwa kwa watoto wenye ulemavu, njiti na wenye matatizo ya ukuaji wa kiakili na kimwili. Jedwali Na.8 linaonesha viwango vya maambukizi ya magonjwa mbalimbali kwa watumiaji waliojitokeza kupata matibabu kwenye hospitali za Muhimbili.

KIUCHUMI:
Matumizi ya dawa za kulevya huongeza mzigo kwa taifa kwa kuwa hupunguza nguvu kazi na husababisha uharibifu wa mali. Vilevile, gharama za udhibiti zikiwemo utoaji wa elimu kwa umma, uteketezaji wa mashamba ya bangi, uendeshaji wa kesi, kuwatunza wafungwa magerezani na kuwatibu watumiaji huongeza mzigo kwa taifa na jamii kwa ujumla.

Biashara ya dawa za kulevya husababisha mfumuko wa bei unaotokana na fedha za biashara hiyo kuingizwa kwenye mfumo halali. Aidha, matumizi ya dawa zakulevya husababisha utoro mashuleni au kazini, kusitisha masomo au kufukuzwa kazi. Kwa ujumla, matumizi na biashara ya dawa za kulevya vimeendelea kuchangia kuongeza umaskini nchini.

KIJAMII:
Dawa za kulevya zimeendelea kusababisha mmomonyoko wa maadili katika jamii. Utumiaji na biashara ya dawa za kulevya mitaani husababisha tabia hiyo kuzoeleka na hivyo kuwavutia watu wengine hasa watoto kujiingiza kwenye tatizo hilo na kuchangia kuharibika kwa kizazi kijacho.Aidha, matumizi ya dawa ya hizo huchangia migogoro ya kifamilia katika jamii jambo linaloweza kuzisambaratisha kabisa. Wazazi ambao hutumia dawa za kulevya, huonesha mfano mbaya kwa watoto wao na jamii kwa ujumla. Pia, kumekuwepo na ajali zilizosababishwa na uendeshaji wa magari na mashine huku waendesha vyombo hivyo wakiwa wametumia dawa za kulevya. Ajali hizo mara kwa mara zimekuwa zikisababisha ulemavu na vifo vingi. Wajidunga hutupa ovyo mabomba ambayo huweza kusababisha majeraha kwa wapita njia au maambukizi ya magonjwa mbalimbali.

Watumiaji wamekuwa wakijihusisha na tabia na vitendo viovu vikiwemo wizi, uporaji, biashara ya ngono na ubakaji. Jamii imekuwa ikiamini kuwa matumizi ya dawa za kulevya ni jambo la kujitakia, hivyo kuwanyanyapaa na kuwabagua watumiaji. Vitendo na muonekano wao huwafanya wasikubalike katika jamii jambo linalosababisha kuendeleza vitendo vyao vya uhalifu na utumiaji wa dawa za kulevya. Halikadhalika, kosa la kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya huambatana na adhabu kali ikiwemo kifungo cha maisha jambo ambalo linawatenga wahusika na familia zao pamoja na jamii. Biashara ya dawa za kulevya huhusisha rushwa kubwa ambayo huathiri utoaji haki kwa wananchi na utawala bora. Wafanyabishara wa dawa za kulevya hutumia sehemu ya faida wanayopata kusaidia jamii ambayo huwaonea aibu kuwachukulia hatua pindi wanapojihusisha na vitendo viovu.

Wafanyabiashara hujitumbukiza kwenye vitendo vya kihalifu kama utekaji nyara, ugaidi, mauaji ya kikatili, vita vya wenyewe kwa wenyewe na ujambazi, hivyo kusababisha uvunjifu wa amani. Vilevile, wafanyabiashara wa dawa za kulevya huweza kuwarubuni watendaji wa vyombo vya udhibiti wa dawa za kulevya kuvujisha siri hivyo kuhatarisha maisha ya watendaji na raia wema.

KISIASA:
Wafanyabiashara wa dawa za kulevya huweza kuwashawishi wapiga kura kwa kutumia rushwa kuwachagua viongozi watakaosimamia maslahi yao pindi watakapokuwa madarakani. Biashara ya dawa za kulevya huweza kuchochea machafuko ya kisiasa na kuweza kupindua serikali iliyopo madarakani. Halikadhalika, nchi inayojihusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya huharibu taswira ya nchikimataifa na kusababisha madhara mbalimbali ikiwemo raia wake kutoaminika na kupata usumbufu mkubwa wanapokuwa kwenye nchi nyingine.

KIMAZINGIRA:
Kilimo cha bangi kinachofanyika kwenye vyanzo vya maji na kwenye ardhi oevu husababisha kukauka kwa mito na kuleta ukame. Pia, ukataji miti ovyo na uchomaji moto wa misitu kwa ajili ya kuandaa mashamba ya bangi husababisha mmomonyoko wa udongo.

NB:
Kila ifikapo tarehe 26 mwezi wa 6 kila mwaka,hua ni siku ya kupiga vita matumizi ya dawa za kulevya duniani.

0 comments:

Chapisha Maoni