• TANZAKILIMO TANZANIA

    Pata taarifa sahihi kuhusu kilimo na ufugaji,kwa weledi wa hali ya juu

  • WATAALA WA KILIMO NA UFUGAJI

    Tunakupatia ushauri wa kitaalam katika maswala yote ya kilimo na ufugaji,toka kwa wataalam wetu waliobobea kwenye nyanja nzima ya kilimo. Wasiliana nasi kwa simu namba +255 675 117 151.

  • UNATAFUTA MASOKO YA MAZAO YAKO? UNATAFUTA MAZAO YA KUNUNUA?

    Tanzakilimo inakuunganisha na wakulima/wanunuzi na wadau wote wa maswala ya kilimo. Wasiliana nasi leo tukuunganishe na wadau....

Jumatano, 26 Desemba 2018

KUWA MILIONEA KWA KULIMA TANGAWIZI


Tangawizi ni aina ya zao la kiungo ambalo sehemu inayotumika ni tunguu (rhizome) ambalo huonekana kama mizizi ya mmea. Asili ya zao hili ni maeneo ya kitropiki ya bara la Asia na hasa katika nchi za India na China.


Zao hili linazalishwa kwa wingi kutoka katika nchi ya Jamaica. Hapa nchini zao hili hulimwa katika mikoa ya Kigoma, Tanga, Morogoro, Pwani, Mbeya na Kilimanjaro.

Tangawizi hutumika kama kiungo katika kuongeza ladha, harufu na kuchangamsha katika vinywaji (kama chai, soda, juisi, vilevi n.k) na vyakula mbalimbali kama mikate, biskuti, keki, nyama za kusaga, achari n.k. Hutumika pia katika viwanda vinavyotengeneza madawa ya tiba mbalimbali kama dawa za meno, kikohozi, tumbo na muwasho wa ngozi n.k. pia hutumika katika vipodozi kama poda n.k).


AINA ZA
TANGAWIZI 

Hakuna uthibitisho wa aina za tangawizi ambazo
hulimwa hapa nchini ila kuna dalili ya kuwa na aina za White Africa (Jamaica)
na Cochin (flint); hii huwa na tunguu ngumu zenye nyuzi.

TABIA YA MMEA 
Tangawizi ni mmea unaotambaa chini ya ardhi,
wakati wa masika hutoa majani juu ya ardhi. Jamaica ina rangi hafifu ya kahawia
na tunguu fupi wakati Cochin ina tunguu fupi zaidi lenye ngozi ya rangi iliyo
kati ya kijivu na nyekundu. Mmea una urefu wa futi mbili na majani yake ni
membamba marefu ambayo hufa kila mwaka yakiacha tunguu ardhini likiwa hai. Maua
ya mmea huu yana rangi nyeupe au manjano.

HALI YA HEWA NA
UDONGO 
Zao hili hustawi katika maeneo yenye hali ya
kitropiki, kutoka usawa wa bahari hadi mwinuko wa mita 1,500 au zaidi. Huhitaji
mvua kiasi cha mm.1,200-1,800 na joto la wastani wa nyuzi za sentigredi 20-25.
Hustawi vema katika udongo tifutifu wenye rutuba na usiotuamisha maji.

MMEA WA TANGAWIZI

UPANDAJI 
Zao la tangawizi hupandwa kwa kutumia vipande
vya tunguu vyenye kichipukizi kizuri angalau kimoja na huweza kukatwa katika
urefu wa sm.2.5-5. Wakati mwingine, vichipukizi vinavyopatikana katika kumenya
tangawizi huweza kuhifadhiwa na kutumika kwa kupanda. Kiasi cha kilo 840-1700
cha vipande vya tunguu huweza kutumika kwa kupanda katika hekta moja. Nafasi
inayotumika kupanda ni kati ya sentimita.23-30 kwa 15-23 na kina cha
sentimita.5-10 na mara nyingi hupandwa katika matuta. Baadhi ya mazao huweza
kupandwa katika shamba la tangawizi ili kuweka kivuli chepesi ingawa si lazima
kivuli kiwepo. Inashauriwa kumwagilia maji endapo mvua inakosekana.

Wiki 1-2 kabla ya kupanda weka mbolea ya samadi
au mboji kiasi cha tani 25-30 kwa hekta na kwa kukuzia weka kiasi cha NPK kwa
uwiano wa kilo 36:36:80. Tandaza nyasi shambani kuhifadhi unyevunyevu hasa pale
kivuli kinapokosekana. Palizi hufanywa mara magugu yanapoota, dawa ya kuua
magugu, kama simazine au round up hutumika.

Magonjwa na
wadudu: 
• Madoa ya majani yanayosababishwa na
viini vya magonjwa viitwavyo Colletotrichum zingiberis na Phyllosticta
zingiberi.
• Kuoza kwa tunguu; kunasababishwa na
viini viitwavyo Pithium spp
• Mizizi fundo; inasababishwa na
Meloidegyne spp.

UVUNAJI 

Tangawizi huweza
kuwa tayari kwa kuvuna kati ya miezi 6-10 baada ya kupanda, wakati majani yake
yanapogeuka rangi kuwa njano na mashina kusinyaa. Tangawizi inayohitajika kwa
kuhifadhi kwenye kemikali (preserved ginger in brine) huvunwa kabla haijakomaa
kabisa, wakati ile iliyokomaa kabisa huwa kali zaidi na huwa na nyuzi hivyo
hufaa kwa kukausha na kusaga. Mavuno hutofautiana kulinganana na huduma ya zao,
mavuno yanaweza kuwa kiasi cha tani 20-30 cha tangawizi mbichi huweza
kupatikana.

USINDIKAJI 

Tangawizi
ikisindikwa utapata unga, mafuta maalum (essential oils) n.k. Tangawizi
iliyovunwa huweza kumenywa, kukatwa na kukaushwa juani au mara nyingine
huchovywa katika maji yaliyochemka kwanza na ndipo kukaushwa au hukamuliwa
mafuta. Pia tangawizi husindikwa na kuhifadhiwa kwenye chupa zikiwa
zimechanganywa na sukari na/au chumvi au bila kuweka kitu chochote. Hata hivyo
tangawizi ina Kiasi cha mafuta cha 16.0-18.0%.

GHARAMA ZA
UZALISHAJI NA MAPATO


Gharama ya hekari moja

Kukodi shamba Tshs.=100,000/=

Mbegu 200, 000/=


Kulima 100,000/=

Kupanda 100,000/=

Kupalilia x 4 @ 90,000/= jumla = 360,000/=

Mbolea / samadi 150,000/=

Jumla 1,010,000/=

Mapato kwa hekari.

Ekari moja ya maandishi inatajwa kutoa kilo 8,000 hadi 10,000. Katika hali halisi, kwa uzoefu wangu, ekari moja hutoa kati ya kilo 4000 hadi 6,000. Kutegemeana na kama umeandaa shamba kwa wakati, umefanya palizi kwa wakati, uwepo wa mvua za kutosha na hali ya rutuba ya shamba lako.

Ghalama hizi hutegemea sana na msimu zinaweza shuka au kupanda zaidi.





MASOKO





Sokoni tangawiz huuzwa sh 5000 mpaka 6000 kwa kg soko linapokua zuri, pia kuna msimu hushuka bei mpaka sh 2000 kwa kg.





Kwa masoko ya Tangawizi wasiliana nasi kwa simu namba 0675 117 151, nasi tutakutafutia msoko ya uhakika.



Alhamisi, 6 Desemba 2018

viatamishi (incubators)




Wafugaji wengi wanaonesha kuvutiwa na njia ya utotoleshaji wa mayai unaofanywa na mashine maalumu za kutotolesha mayai maarufu kwa jina la viatamishi (incubators) .Wengi wana kiu ya kutaka kujua gharama, faida, hasara na upatikanaji wa mashine hizi.Kwa kuthamini mchango wa wafuatiliaji wa website hii, nimelazimika kuitumia wiki hii kulielezea hili swala kwa upana wake.

.Viatamishi ni nini?   Hizi ni mashine maalumu zinazotumika kurahisisha utotoleshaji wa mayai ya aina zote  ya kuku wa asili na wale wa kisasa. Pia, inaweza kutumika kwa mayai ya kwale, bata na kanga.Mashine hizi hutofautiana ukubwa, lakini pamoja na tofauti hiyo, bado kila moja ina uwezo wa kutumia muda mfupi kutotolesha mayai, tofauti na muda anaoutumia kuku kuatamia hadi kupata vifaranga.Aina za viatamishiKwa jumla, mashine hizi zote zina kazi moja tu ambayo ni utotoleshaji, japo zimetofautishwa kwa mifumo yake ya kiuendeshaji.Mfumo wa kwanza unazijumuisha mashine zote zinazototolesha mayai kwa kujiendesha zenyewe(automatic).Mfumo wa pili unaziunganisha mashine zote zinazofanya kazi kwa kuendeshwa kwa msaada wa kibinadamu.

Mashine zinazojiendesha zenyewe zinatumika sana kibiashara kwa sababu zinarahisisha kazi tofauti na ilivyo kwa zile zinazoendeshwa na binadamu.Mashine hizi zina faida kubwa kwani si rahisi kuharibu mayai kutokana na kuwa na mashine ndani ambayo kazi yake ni kusaidia kutawanya joto kwenye mayai.Uzuri wake ni kwamba hata joto likizidi uwezekano wa kuharibu mayai haupo kwa sababu feni inasaidia kupunguza joto ndani ya mashine.Kundi la pili linajumuisha mashine zinazofanya kazi zake kwa kutumia uwapo wa mtu muda wote.Aina hii ya mashine hutumia upepo wa kawaida kuendesha zoezi la utotoleshaji, haina feni maalum lakupoza joto.Hii ina maana lazima mtu awe karibu na mashine wakati wote wa utotoleshaji ili aweze kufanikisha mchakato wote.Sifa za viatamishi Kama nilivyotangulia kusema hapo awali kuwa mashine hizi hazitofautiani sana, ukiachilia mbali ukubwa na mfumo wa uendeshaji. Zipo mashine zenye uwezo wa kutotolesha mayai mengi zaidi kwa pamoja, na nyingine kulingana naudogo wake zinalazimika kutotolesha mayai machache kwa muda mfupi pia.Kwa kawaida mashine nyingi za utotoleshaji hutumia umeme kidogo wa unaokadiriwa kuwa waVoltage:110V- 220V.Ukifanikiwa kupata mashine bora, unajijengea uhakika wa kutotolesha asilimia 95 ya mayai yote.

Unazijuaje mashine bora? Si jambo rahisi kuzijua mashine bora, lakini unaweza kutazama baadhi ya vitu muhimu kama vile tochi maalumu yenye uwezo wa kukagua uhai wa mayai yaliyomo ndani ya mashine.Zipo mashine zenye uwezo wa kila trei ya mayai kuwa na sehemu ya kuangulia vifaranga, kuangalia mfumo maalumu ‘full Automatic’ unaoweza kugeuza mayai, kudhibiti joto na unyevu ndani ya mashine.Jambo muhimu zaidi ni kuhakikisha unatumia mashine yenye uwezo wa kutunza joto kwa muda wasaa sita mara baada ya umeme kukatika.

Viatamishi vya mafuta :Ni muhimu pia kueleza kuwa mbali ya nishati ya umeme, viko vitamishi vinavyoweza kujiendeshakwa kutumia nishati ya mafuta kama ya taa au petrol. Kwa kawaida aina hizi za viatamishi huwa na gharama ndogo.Kwa Watanzania na hata viwanda vidogo vimekuwa vikitengeneza aina hizi za viatamishi. Ni muhimu kutafuta taarifa za viatamishi hivi kutoka kwa wataalamu wa ufugaji au wafugaji wakubwa.



Jumapili, 23 Septemba 2018

UFUGAJI BORA WA SAMAKI


Ufugaji wa samaki unakua kwa kasi sana hapa nchini tanzania kutokana na kuonekana kua na faida sana. hivyo nimeamua leo nikupe elimu kidogo ambayo itakusaidia wewe mfugaji ambaye ungependa kujikita katika ufugaji huo.


SIFA ZA ENEO LA KUFUGIA SAMAKI
Sio kila mahali hufaa kwa ufugaji wa samaki, ila mahali ambapo ni sahihi, zifuatazo ni sifa za eneo bora la kufugia samaki.


  • eneo linalo fikika kwa urahisi

  • eneo tulivu na lenye usalama wa kutosha

  • eneo ambalo linavibali vyote vya umiliki

  • lazima liwe na maji ya kutosha kwa kipindi chote utakacho fuga

  • eneo ambalo halina mmomonyoko wala historia ya mafuriko

  • eneo lenye uwezo wa kutuamisha maji

  • eneo ambalo soko lake sio la shida
    UTENGENEZAJI WA BWAWA
    Kuna aina mbali mbali za kutengeneza mabwawa ya samaki inategemea na eneo, kiasi cha samaki unao taka kufuga, aina ya samaki na hali ya uchumi.aina hizo ni

    • bwawa la kuchimba udongo bila kujengea(earthen pond)







    • bwawa la kuchimba na kujengea 


      



     UPANDIKIZAJI WA VIFARANGA/MBEGU ZA SAMAKI KATIKA BWAWA

    Kabla vifaranga hawaja safirishwa ni vyema kuwatoa katika bwa kubwa wanalo ishi na kuwaweka katika vibwawa vidogo vidogo  kati ya masaa 24 hadi 72 kuendana na umbali wa safari bila kuwapa chakula chochote kile.



    • baada ya kuwasafirisha mfugaji  atakiwi kuviweka kwenye bwawa moja kwa moja ila inatakiwa maji yalio tumika katika kuwasafirisha yabadilishane joto na maji ya bwawa ambalo wataenda kuishi. hivyo mfugaji anatakiwa kuliweka kontena ambalo vifaranga wamo ndani ya bwawa ambalo wataishi kwa dakika 30 hadi 35 bila kuwafungulia, baada ya hapo kontena liina mishwe taratibu ili kuwezesha maji ya bwawa na yaliyo kwenye kontena kubadilishana na baadae vifaranga watatoka taratibu,


    endapo hautafanya hivyo  unaweza kusababisha vifaranga vyote kufa kutokana na mabadiliko   ya joto ambayo yanaweza kutokea ghafla.




    • unatakiwa kusafirisha vifaranga wako mda ambao hali ya hewa inakua sio joto yaan mda wa jion na asubuhi ili kuwezesha vifaranga kuimili misukosuko ya safari na bila kupatwa na joto kali.


    CHAKULA NA UTUNZAJI WA SAMAKI BWAWANI

    • Samaki hutakiwa kupewa chakula angalau mara 2 kila  siku  unatakiwa kuzingatia mda sahihi wa kuwapa chakula yaan asubuhi saa 3-4 na jion saa 9 -10 samaki upewa vyakula tofauti kulingana na aina
      tabia ya ulaji wa samaki ni kama ifuatavyo 



      1. samaki wanao kula nyama (sangara, kambale)

      2. samaki wanao kula mimea carps

      3. samaki wanao kula mchanganyiko (perege,sato na samaki wa maji ya chumvi mfano kibua)


      zingatia kuweka maji  ambayo ni safi 



      TARATIBU ZA ULISHAJI WA SAMAKI


      UMRI(wiki)                          UZITO(gm)             KIASI CHA CHAKULA KWA SIKU (gm)

      1-2                                           5-10                                   1

      2-3                                           20-50                                 2

      3-5                                           50-110                              3

      5-7                                            110-200                           4

      7 nakuendelea                          200 na zaidi                     5



Ijumaa, 7 Septemba 2018

FAIDA NA HASARA ZA KUTUMIA KILIMO CHA GREEN HOUSE


GREEN House, kwa tafsiri isiyo rasmi, ni nyumba kitalu. Nyumba ambayo imejengwa kukidhi mahitaji ya mimea. Nyumba hizi hujengwa kwa ustadi mkubwa wa kitaalumu kwa kuzingatia baadhi ya mambo muhimu.

Baadhi ya mambo hayo muhimu ni pamoja na hali ya hewa ya eneo husika joto, baridi, mwanga wa jua, uelekeo wa upepo, muinuko kutoka usawa wa bahari, aina ya udongo, ubora wa maji, mteremko wa eneo husika.

Lakini pia kuna mambo ya kuzingatia kama aina za malighafi za kutumika na ubora wake nailoni, neti kivuli, mbao au chuma, plastiki, upatikanaji wa maji, kufikika kwa eneo, muinuko wa jengo (Gutter height), ni muhimu kuzingatia urefu kutoka usawa wa ardhi kabla ya kuezeka green house

Mazao yanayooteshwa kwenye mfumo huu yako ya aina maalumu kwa maana ya aina ya mbegu za kutumika/hybrid/F1, zenye sifa mbalimbali kama urefu, ipo namna yake ya uwekaji mbolea, kumwagilia ambazo ni njia tofauti sana na inavyofanyika katika mashamba ya wazi.

Sababu za watu kupenda kutumia aina hii ya kilimo

Kwanza kabisa sababu kubwa inayowasukuma wengi kuingia katika kilimo hiki ni ile ya kutoa mavuno mengi katika eneo dogo, kwa mfano kuna taarifa ambazo huenezwa na watu kuwa unaweza kupata tani 60 za zao kama nyanya ndani ya green house kwa eneo la upana wa mita 8 na urefu wa mita 15.

Aina hii ya taarifa ni moja ya kichocheo ambacho huwavutia sana watu, kwani mtu hupiga haraka hesabu za mapato na kuona kuwa inalipa.

Pia taarifa nyingine ambazo huwatia watu faraja na matumaini juu ya kilimo hiki ni kwamba ni aina ya mfumo ambao hauna usumbufu badala yake mtu hujipatia fedha zake kwa haraka.

Ukiacha taarifa za namna hiyo pia zipo zile zinazosema kuwa ukimaliza kujenga tu jengo la Green House, basi wewe ni tajiri yaani utakuwa na kazi ya kupanda na kusubiri kuvuna tu hata kwa miaka 10 mfulululizo.

Kwa taarifa kama hizi hufanya mtu kuwaza mapato makubwa, kuwa ikiwa kwa labda miezi 3 tu nina tani 60 za nyanya kwa eneo la mraba la mita 120, na anaambiwa unavuna tu, na jengo ni imara linadumu kwa miaka 10 bila matengenezo wala marekebisho.

Pamoja na kwamba aina hii ya kilimo imekuwa na faida lakini pia imekuwa na changamoto zake zinazowakumba wakulima wanaotumia mfumo huu wa kilimo.

Kwa maeneo ya miji mikubwa kama, Dar es Salaam na mikoa mingine zipo baadhi ya green house ambazo zimejengwa mwaka jana, lakini wamiliki wake wamezitelekeza na wengine wamezibomoa baada ya kuona wanapata mashambulizi ya magonjwa na wadudu.

Wapo baadhi ya wakulima kwa kupata taarifa zisizo sahihi waliaminishwa kuwa hakuna magonjwa wala wadudu wanaoshambulia mazao yaliyopo ndani ya green house, hivyo wakulima wakaishi kwa kujiamini kwa kujua kuwa wanachosubiria ni mapato ya tani 60.

Matokeo yake wamejikuta wanapata magonjwa na wadudu kama mazao ya shamba wazi, unakuta ni green house ya nyanya lakini ndani unakuta kuna changamoto ya wadudu.

Kuna baadhi ya wakulima mazao yao yamenyauka na kufa yakiwa ndani ya green house, kuna wakulima walijenga green house kwa matumaini ya kupata pesa ya haraka na wameishia kupata hasara kwa kuwa hawakupata ushauri sahihi na mazao yao yamekauka pia kama vile yapo kwenye shamba la wazi.

Mara nyingi green house hizi zimekuwa kwenye eneo lenye joto kubwa ikilinganishwa kuwa kimo chake kinapaswa kuwa chini ya mita 2.5, hivyo kufanya joto kuwa kali sana na mazao kunyauka, ambapo wataalamu wanashauri kuwa ni bora zaidi kujengwa kulingana na mazingira ya eneo au mkoa husika.

Mavuno kidogo.

Wapo wakulima waliolima ndani ya green house, mbali ya kwamba walikuwa wakiaminishwa kuwa watapata mavuno mengi yatakayowafanya kurudisha gharama zao ndani ya msimu mmoja matokeo yake imekuwa kinyume kabisa (mavuno hafifu na yasiyo bora) jambo ambalo linatokana na kutozingatia kanuni bora za uandaaji wa aina hii ya kilimo.

Kukosekana kwa soko

Baadhi ya wakulima waliowekeza kwenye kilimo hiki wamekuwa wakiaminishwa kuwa kwa kuwa ni mavuno ya green house, basi yatapata soko zuri muda wowote atakaovuna, jambo ambalo ni kinyume ambapo kwa sababu hizo wamekuwa wakizalisha mazao bila ya kuwa na hofu ya kukosa soko.

Na hivyo kujikuta kwamba pindi inapofikia wakati wa mavuno imekuwa kilio kwani mazao hayo yamekuwa yakipata bei sawa tu na yale ya mashamba ya kawaida huku wakati mwingine mazao hayo yakiharibika kabisa kwa kukosa soko.

Ubora hafifu wa mazao

Kwa mujibu wa wataalamu wanabainisha kuwa mazao huwa si mazuri na kutofanana hatua zote za ukuaji.

Kwani baadhi ya wakulima waliaminishwa kuwa mazao yote yaliyomo ndani ya green house yatakuwa katika kiwango sawa na yatafanana kwa kuwa yapo katika mazingira mazuri ya aina moja.

Hivyo kumfanya mmiliki kuamini kuwa kwa kuwa ni green house ni lazima ukuaji uwe bora na mzuri, hata kama hatofanya jitihada zozote, yeye atasubiri kuvuna na kupata pesa tu.

Ili kuweza kufanikiwa kwenye kilimo hiki cha green house basi kuna mambo ya kuzingatia kabla ya kuingia katika aina hii ya kilimo.

Wataalamu wa kilimo hiki wanasema kuwa kwanza kabisa ili mtu aweze kufanikiwa basi hana budi kuhakikisha kuwa anaweka juhudi, umakini na malengo katika jambo husika, kwani unaweza kuwa na green house lakini bado ukaambulia hasara na usifaidike na chochote kinyume na matarajio yako.

Na hivyo kwa sababu hiyo ukajikuta uko sawa tu kama siyo nyuma ya yule aliyelima kilimo cha kawaida ambacho ni cha wazi.

Lakini pia jambo jingine la kuzingatia ni kuhakikisha kuwa unafahamu vizuri kilimo hiki, ikiwamo pia kutambua mbegu zilizobora na zinazoendana na soko unalolilenga kwani kinyume na hivyo unaweza kujikuta unaambulia hasara.

Hivyo ni busara kabla ya kuanza aina hii ya kilimo ni vizuri iwapo utatafuta ushauri kwa watu waliokwisha kufanikiwa kupitia mfumo huu lakini pia kutafuta taarifa mbalimbali juu ya aina hii ya kilimo.

Hii itakusaidia kujua changamoto na namna gani unavyoweza kuzikabili ikiwamo, gharama, magonjwa kwani usipokuwa makini unaweza kujikuta unakabiliana na changamoto zilizoko kwenye kilimo cha kawaida cha shamba wazi ilihali una green house.

Pia jambo jingine la kuzingatia ni kuhakikisha kuwa unafanya utafiti wa kina kabla ya kuamua kuingia kwenye aina hii ya kilimo, hii itakusaidia kuweza kulibaini soko linavyokwenda na upande na kuvuna wakati gani.

Pia hakikisha kuwa unapata fundi ambaye ni mzoefu kwenye uandaaji huu wa green house ikiwamo kujiridhisha kwanza kuhusu ubora wa kazi zake alizowahi kufanya kabla ya kuingia makubaliano ya kukutengenezea green haouse yako.

Jumatatu, 13 Agosti 2018

HIZI NDIZO SABABU ZA KUKU WAKO KUDONOA MAYAI NA KUDONOANA


Kati ya mambo ambayo mfugaji anatakiwa kuwa nayo makini ni pamoja na tabia za kila siku za mifugo yake. Kuna wakati kuku wanakuwa na tabia za kudonoa na kula mayai,pia kudonoana wenyewe kwa wenyewe. Tabia hii si nzuri na si ya kawaida. Hizi hapa chini ni sababu zinazopelekea kuku kuwa na tabia hizi:

SABABU ZA KUKU KULA MAYAI.

1. Ukoo- Hapa utakuta ndo ukoo/uzao wao wanatabia ya kula mayai hivyo kuku hufanya muendelezo wa kula mayai,

2. Kuto kupata chakula cha kutosha- Hii ni moja ya sababu kubwa kabisa inayo pelekea kuku kula mayai,chakula kikiiwa kichache hawashibi hupeleka kutafuta njia mbadala ya kushiba. 

3. Kukosa madini joto- Hii inaweza kuwa ndo sababu kuu ya kwa nini kuku wanakula mayai, kuku wakikosa madini joto ni lazima wale mayai na hata kulana wao wenyewe, na jua kwamba kwenye yai kuku huwa anatafuta lile ganda la juu pekee sema anapo donoa na kulipasua yai hujikuta anakula na ute na kiini ila yeye lengo lake hasa ni ganda la juu.

 4. Kuku kutagia sehemu nyeupe sana yenye mwanga mkali upelekea kuku kula mayai,kuku anapenda kutagia sehemu fichifichi yenye mwanga hafifu kidogo ndo anakua huru zaidi kutaga.

5. Mayai kukaa muda mrefu bila kukusanywa baada ya kutaga- Hapa ni kwamba mayai yanapo kaa muda bila kukusanywa na kama yapo sehemu ya wazi ni rahisi wao kudonoa.

6. Lishe mbaya-kuku akipata lishe mbaya ya chakula humpelekea kudonoa chakula,kuku anapaswa kupata chakula chenye virutubisho vyote.

7. Nafasi ndogo-kuku wanapaswa kupata nafasi kubwa yakupumzika na kulia chakula.

8. Vyombo vichache-bandani unapaswa kuwa na vyombo vya chakula na maji vya vyakutosha kuondoa kusukumana na kutokula kwa raha.

9. Kukosa shughuli yakufanya-kuku wakila wakishiba unapaswa kuwafungia majani km kabeji ili wawe bize mda wote.

NAMNA YA KUZUIA KUKU KUDONOANA AU KULA MAYAI 

1. Chakula cha kutosha ni muhimu sana, ili kuwafanya wasitake kula mayai ili kushiba.

 2. Mayai yakusanywe mara tu anapo taga na usiyaache muda mrefu bandani. 

3. Sehemu ya kutagia iwe na giza la kutosha ili kufanya kuku ashindwe kuona yai alilo taga.

4. Madini joto ni muhimu sana. 

5. Kuku wenye tabia za kula mayai unaweza chinja au kuuza. 

6. Kuweka idadi ya kuku inayolingana na sehem ulionayo.

 7. Usizidishe mwanga. 

8. Banda liwe safi.

9. Weka vyombo vya kutosha. 

10. Wape lishe bora

11. Wape kuku shughuli kwa kuwawekea bembea na sehemu ya uwazi kwa ajili ya mazoezi. 

12. Kata midomo ya juu.

13.Epuka ukoo wenye tabia hizo.

Kwa leo naishia hapa,nakutakia mafanikio mema kwenye ujasiriamali wako, Mungu awabariki sana.
⁠⁠⁠

Jumamosi, 27 Mei 2017

Black Australorp ( Kuku Weusi wa Malawi)


Australorp wanastahimili mazingira tofauti, kama kuku wa kienyeji aliye zoeleka nchini Tanzania. Na ni wazuri kwa ufugaji huria, kwa kuwaachia nje wajitafutie chakula wenyewe. Ingawa wanajulikana kwa sifa yao ya utagaji mayai mengi, lakini kuku hawa wanafaa kwa nyama pia, kwani huwa na nyama nyingi sana (dual purpose chickens)

Kuku hawa huweza kumpatia mfugaji faida kubwa, kwani ni wazuri kwa biashara ya mayai na nyama pia. Hawana sifa nzuri ya kulalia mayai, lakini akilalia hutotoa vifaranga vingi, na ni wazuri kwa uleaji wa vifaranga hivyo.

Utagaji wao wa mayai unakaribia ule wa kuku wa kizungu. Kuku hawa ni wakubwa, wazito, na wanamvuto sana kuwaangalia. Wanapendeza pia kwa ufugaji mdogo, katika mazingira ya nyumbani. Wana michirizi ya kijani pale wanapomulikwa kwenye mwanga mkali wa jua.

Kwa wastani Black Australorp, hufikisha mayai 250 kwa mwaka, wakiwa katika mazimgira mazuri. Kuku hawa ni wapole na rafiki kwa binadamu. Black Australorp ni wagumu, hawapati magonjwa mara kwa mara, hivyo basi huvumilia magonjwa ya aina nyingi, na hawachagui chakula. Wanakula vyakula wanavyo kula kuku wengine wa kienyeji. Huanza kutaga wakiwa na umri wa miezi mitano na nusu hadi sita.

Jogoo hufikisha kilo 3.5 – 5.0 na
Temba/hen hufikisha kilo 3.0 – 3.7

kwa mahitaji ya aina hii ya kuku,wasiliana nami kwa simu namba o716 71729o,tuko kigamboni,dar es salaam

Jumatano, 24 Mei 2017

LISHE YA KUKU NA KUCHANGANYA CHAKULA


LISHE YA KUKU:

Ili kuku waweze kuishi, kukua vizuri, kunenepa na kutaga mayai mengi ni lazima wale chakula kingi na chenye ubora unaotakiwa. Uwingi na ubora wa lishe ya kuku unaweza kuainishwa katika makundi ya vyakula kama ifuatavyo:

  1. Vyakula vya kutia nguvu

  2. Vyakula vya kujenga mwili

  3. Vyakula vya kuimarisha mifupa

  4. Vyakula vya kulinda mwili

  5. Maji.


MAKUNDI YA VYAKULA:





    1. Vyakula vya kutia nguvu:




Vyakula vya mifugo vifuatavyo vinawekwa katika kundi hili;

  1. Pumba za mahindi, pumba laini za mpunga, na, pumba laini za ngano.

  2. Nafaka kama vile mtama , chenga za mahindi ,chenga za mchele, uwele , na ulezi

  3. Mimea ya mizizi kama vile muhogo, viazi vitamu na magimbi. Kabla ya kulisha kuku hakikisha mizizi hiyo inalowekwa kwa muda wa saa moja au kupikwa kabla ya kukausha ili kuondoa sumu ambayo kwa asili imo katika vyakula vya aina hii.Inashauriwa kuwamizizi hiyo ilishwe kwa kiasi cha asilimia 10% ya chakula chote anacholishwa kuku.


Katika kundi hili la kutia nguvu ,vyakula vya mafuta kama vile mafuta ya kutoka kwenye vyakula vya mafuta kama mashudu ya mimea ya mafuta, mafuta ya samaki husaidia kuongeza nguvu na joto mwilini. Vyakula vya kutia nishati huchangia asilimia 60-70 ya mchanganyiko wote wa chakula.

  1. Vyakula vya kujenga mwili:


Ø  Mashudu :Haya ni makapi ya mbegu za mimea aina ya mikunde na vyakula v vinavyotoa mafuta kama vile alizeti, mawese, karanga, soya ,korosho, na ufuta .

Ø  Damu ya wanyama iliyokaushwa (waliochinjwa na kukaguliwa), hii inafanywa ili kuepusha uwezekano wa kuku kupata magonjwa ya kuambukiza .

Ø  Mabaki ya samaki ya samaki/dagaa na nyama.

Ø  Vyakula asilia kama vile minyoo, mayai ya mchwa, Masalia ya nyama toka kwenye ngozi/mifupa, wadudu walioteshwa kutokana na damu au nyama iliyooza na vyakula vya aina nyingine.

Ø  Vyakula hivi huchangia asilimia 20 hadi 30% ya mchanganyiko wote wa chakula cha kuku.

  1. Vyakula vya kuimarisha mifupa(madini): a)Hivi ni vyakula vya madini ambavyo huhitajika kwa ajili ya kujenga mifupa, maganda ya mayai, kukua na kuuweka mwili wa ndege (kuku) katika hali ya afya njema kwa ujumla.

  2. b) Madini ya muhimu ni madini ya chokaa (calcium) na fosiforasi (phosphorus). Ili kuku watage mayai yenye ganda gumu ni lazima wapate madini ya chokaa maganda ya konokono na mayai yaliyosagwa vizuri. Lakini inapendekezwa kwamba unapoongeza madini ya fosforasi inakubidi uongeze pia madini ya chokaa kadri inavyopasa ,kwasababu kiwango cha aina moja kikizidi kuliko cha aina nyingine husababisha upungufu wa kile kidogo


Viinilishe vya madini vinavyotakiwa ni pamoja na;

Ø  Majivu ya mifupa yaliyosagwa vizuri, unga uliosagwa wa magamba ya konokono wa baharini, konokono wa nchi kavu na maganda ya mayai yaliyochomwa . Kabla maganda ya mayai na nyumba za konokono havijatumika inashauriwa yachomwe moto mkali au yachemshwe ili kuua vijidudu vya maradhi.

Ø  Chumvi ya jikoni

Ø  Madini yaliyotengenezwa viwandani kama vile Di-calcium phosphate

Ø  Magadi (kilambo).

  1.     Vyakula vya kulinda mwili:


Kundi hili linajumuisha vyakula vya mbogamboga kama vile;

Ø  Mchicha, samadi ya ng’ombe ambayo haijakaa muda mrefu baada ya kunyewa, mchicha pori, Chinese kabeji n.k.

Ø  na Mchanganyiko wa vitamini uliotengenezwa na viwanda vya madawa (vitamin premix).

Ø  Jua ni muhimu katika kuhakikisha vitamini A na D zinatumika vizuri mwilini, kwahiyo banda ni lazima lijengwe kwa mtindo ambao unaruhusu mwanga kupita hasa nyakati za asubuhi na jioni.

Ø  Chakula cha kuku wanaofugwa ndani ni lazima kichanganywe na vitamini zinazotayarishwa viwandani.

          KUCHANGANYA CHAKULA CHA KUKU:


Njia za kuchanganya chakula cha kuku;

Kuna njia kuu mbili za kuchanganya chakula cha kuku, nazo ni;

Ø  Kuchanganya chakula kwa mashine;

o   Njia hii hutumika viwandani kuchanganya chakula kwa ajili ya kuku wanaofugwa katika mashamba makubwa.

Ø  Kuchanganya chakula majumbani (home made ration): Hii ni njia inayotumika kuchanganya chakula kwa ajili ya kulisha kundi dogo la kuku na njia ambayo inaweza kutumiwa na wafugaji wadogowadogo.

VIFAA; Beleshi /koleo(spade), Turubai/sakafu safi, Viinilishe , Viroba/Magunia kwa ajili ya kuhifadhia chakula kilichochanganywa.

Chakula kilichochanganywa kinaweza kuwekwa katika uzani wa kilo 25-kilo 50, au kilo 100.

                MCHANGANUO WA VIINILISHE VYA CHAKULA CHA KUKU:

 

Aina ya chakula                                   kiasi

  1. Vyakula vya kutia nguvu mwilini:


Ø  Pumba za mahindi            kilo   48

Ø  Pumba laini za mpunga    kilo   26

            Jumla                                            kilo 74

  1.      Vyakula cha kujenga mwili : 


                                       

    MASHUDU YA ALIZETI                                   KILO 18


Damu ya wanyama                                                                    kilo   1

Mabaki ya samaki /dagaa                                                          kilo   3

          JUMLA                                              KILO  22


iii.Vyakula vya kuimarisha mifupa (Madini):

  1. chumvi ya jikoni                                   kilo ½

  2. chokaa(dicalciumphosphate)…            kilo 2

  3. poultry premix/                                     kilo ½

  4.  unga wa mifupa                                  kilo 1


          Jumla                                                      kilo 4

  

Ø  Mahitaji halisi ya viinilishe kwa muhtasari:

Ø  Vyakula kutia nguvu mwilini                             kilo 74

Ø  Vyakula vya kujenga mwili                              kilo 22

Ø  Vyakula vya kuimarisha mifupa (Madini)        kilo 4

  JUMLA                                                                        100

Jumla ya mchanganyiko wa vyakula                kilo 100 

 


HATUA ZA KUCHANGANYA CHAKULA CHA KUKU:


HATUA YA KWANZA:

Katika hatua ya kwanza utaanza kuchanganya vyakula vya madini

Changanya , chokaa, chumvi na majivu ya mifupa pig mix vizuri - huu utauita mchanganyo Na.1

HATUA YA PILI:

Changanya mchanganyo huo na damu pamoja na samaki waliosagwa - huu utauita mchanganyo Na. 2

HATUA YA TATU:

Mchanganyo Na.2 uchanganye na mashudu vizuri ambao utauita mchanganyo Na.3.

HATUA YA NNE:

Mchanganyo Na.3 umwage juu ya rundo la pumba iliyochanganywa (pumba ya mahindi na pumba laini ya mpunga).

o   Chukua beleshi /koleo safi lililo kavu na kulitumia kuchanganya rundo la chakula ili kusambaza viinilishe vizuri.

Mambo ya kuzingatia katika kulisha na kutunza chakula cha kuku:

  1. a) Baada ya kuchanganya chakula kitawekwa kwenye viroba au magunia na kutunzwa ghalani (stoo) hadi pale kitakapohitajika kwa ajili ya kulisha kuku.

  2. b) Hakikisha kuku wanapata lishe kadri inavyopendekezwa na wataalamu.

  3. c) Chakula kilichochanganywa ni lazima kiwekwe sehemu kavu ili kisiharibiwe na unyevunyevu kama vile kwenye chaga mabanzi yaliyotandazwa juu ya mawe yalipangwa vizuri

  4. d) Chakula kilichoharibika hakifai kulisha kuku kwani kinaweza kusababisha matatizo ya afya.

  5. d) Chakula kilichochanganywa kinatakiwa kisikae muda mrefu baada ya kutayarishwa.


Vyakula vya ziada:

Ili kuhakikisha kwamba kuku wanapata viinilishe vya kutosha kuku wanaweza kupewa mchwa na mafunza.

Vilevile vitu mbadala aina ya nafaka vinavyopatikana hutegemea sana aina ya mazao yanayolimwa katika eneo husika.

Mbinu za kuotesha mchwa na funza: Funza na mchwa ni chakula kizuri na rahisi chenye viinilishe aina ya protini kwa kuku wanaofugwa kwa mfumo huria unaoboreshwa. Hata hivyo vyanzo hivi vya chakula cha protini huchangia tu vile ambavyo kuku wanatakiwa kupewa.

  1. Inashauriwa uwape vifaranga hao funza na mchwa kwa sababu ndio wanaohitaji protini kwa kiasi kikubwa na cha kuaminika.


Funza na mabuu yanaweza kuoteshwa kwa njia rahisi na kutumika kuboresha chakula cha vifaranga.

  1. c)Mafunza na mabuu yanaweza kuoteshwa kwa kutumia damu, viungo vya ndani ya tumbo la ng’ombe pamoja na samadi ya ng’ombe.

  2. d) Chungu kijazwe maji theluthi moja ya ujazo wake, inzi watakuja na kutaga mayai katika mchanganyiko ambao mafunza walioteshwa wataanza kula mchanganyiko huo.

  3. e) Baada ya hapo vitu hivi vyote vitachanganywa pamoja katika chungu kimoja kikubwa ambacho kitaachwa wazi wakati wa mchana na kufunikwa wakati wa usiku.

  4. f) Siku tano baadaye maji yatajazwa kwenye mtungi huo na mafunza yatakusanywa wakiwa wanaelea juu. Baada ya kukusanya waoshe vizuri na maji halafu lisha kuku moja kwa moja.

  5. g) Kumbuka kuweka chungu kinachooteshwa mafunza kuweka mbali na maeneo ya watu ili kuepuka harufu inayoweza kusumbua watu.


                                                  KULISHA KUKU:  
 

Makadirio ya chakula cha kuwalisha vifaranga 100/siku moja:






































Umri (wiki baada ya kuzaliwa)Idadi ya

vifaranga
Kiasi kinachotakiwa

Kwa siku moja(kilo)
11001
21001
31002
41003
51004
61005

Maelezo kwa ufupi  kuhusu kulisha kuku:

  • Ni vigumu kukadiria mahitaji ya chakula cha kuku wanaojitafutia chakula, lakini inakadiriwa kuwa kuku mmoja mkubwa wa uzito wa kilo 1-2 anahitaji chakula chenye uzani wa gramu 80-160 kwa siku kwa kuku wanofugwa ndani lakini wale kuku wanafugwa kwa mfumo wa huria nusu huria mahitaji yanakadiriwa kupungua hadi kufikia gramu 30-50 kwa siku .

  • Ifahamike pia kuwa kiasi cha chakula hutegemea mahitaji kutokana na uzito na uzalishaji, mfano kuku anayetaga na anayekua wanahitaji chakula kingi zaidi ya wale ambao hawatagi au wamekoma kukua.

  • Hakikisha kuku wanawekewa chakula na maji safi kwenye vyombo safi na kubadilisha kila vitakapoisha.